.

Jumatatu, 18 Julai 2016

Abakwa na watu 5 kwa mara ya pili India


Kwa mtazamo wa wengi radi haiwezi kupiga mti mmoja mara mbili.,,, lakini kwa mwanamke mmoja nchini India hilo ndilo lililomkuta.

Binti huyo mwenye umri wa miaka 21 amebakwa na wanaume watano kwa mara ya pili.

Miaka mitatu iliyopita binti huyo alibakwa na wanaume hao hao watano katika mji wa Bhiwani.

Sadfa ni kwamba binti huyo aliyetorokea mji tofauti wa Rohtak ulioko katika jimbo la Kaskazini la Haryana alishikwa na kubakwa tena juma lililopita.

Alikuwa akitembea barabarani kisha akatekwa nyara na watu ambao nusura wamnyonge.

Alinusurika kufa lakini alichokipitia ni cha kutamausha sana.

Binti huyo alibakwa na kutupwa kichakani.

Kwa bahati nzuri msamaria mwema aliyekuwa akipita eneo hilo alimsikia akitoa sauti hafifu na kumpeleka hospitalini alikotibiwa hadi akarejesha afya yake.

Alipopata afueni alisema maneno yaliyoibua hasira miongoni mwa jamii.

''Nilikuwa nikitembea barabarani nikitoka chuoni kuelekea nyumbani kisha nikawaona walewale wanaume walionibaka huko Rohtak.

Nilishtuka na kuhofia maisha yangu.

Walishika na kujaribu kuninyonga, walinieleza kuwa watawaua babangu na kakangu.''

Sijui walikonipeleka kwa sababu nilipoteza fahamu ila ninachokijua ni kuwa walikuwa wale wale walionibaka miaka mitatu iliyopita.'' binti huyo kutoka jamii maskini aliiambia runinga moja ya kitaifa nchini India.

Familia yake inasema kuwa washukiwa hao walikuwa wakiwashinikiza kukomesha mashtaka dhidi yao lakini binti yao akakataa kata kata.

Sasa polisi wametumwa huko kuwasaka watuhumiwa hao.

Mamia ya wenyeji wa mji wa Rohtak, wameandamana wakitaka serikali iwachukulie hatua kali washukiwa hao wa kosa hilo la kinyama

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni